Afisa Masoko wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Wilaya ya Mbinga (MBIFACU), Osmund Mbunda, amesema chama hicho kinaendelea kuongeza thamani ya zao la kahawa kwa kusindika na kuuza kahawa iliyotayari kwa matumizi badala ya kutegemea uuzaji wa kahawa ghafi pekee.
Mbunda ameyasema hayo Agosti 3, 2026, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika banda la MBIFACU kwenye Maonesho ya Kilimo Nanenane Kitaifa yanayoendelea jijini Dodoma.
Amesema MBIFACU kwa sasa huuza kahawa katika aina mbalimbali ikiwemo kahawa kavu, kahawa safi na kahawa iliyoongezwa thamani kwa kusindikwa, hatua inayolenga kuongeza mapato ya chama na wakulima pamoja na kuwafanya Watanzania kutumia kahawa zaidi badala ya chai.
Ameongeza kuwa kuongeza thamani ya kahawa ni njia muhimu ya kukuza soko la ndani na kuongeza ushindani wa bidhaa za kahawa katika masoko mbalimbali.
Mbunda amesema ubora wa kahawa unaanzia shambani na si sokoni, hivyo amewahimiza wakulima kuzingatia kanuni bora za uzalishaji kuanzia hatua za awali ili kupata kahawa yenye viwango vinavyokubalika.
Ameongeza kuwa MBIFACU inalenga kuhakikisha Wilaya ya Mbinga na Mkoa wa Ruvuma vinaendelea kuwa vinara wa uzalishaji wa kahawa aina ya Arabica nchini ifikapo mwaka 2050, akibainisha kuwa Ruvuma kwa sasa ndiyo mkoa unaoongoza kwa uzalishaji wa Arabica na unashika nafasi ya pili kitaifa kwa uzalishaji wa kahawa baada ya Mkoa wa Kagera unaozalisha kahawa aina ya Robusta.
Amewaalika wananchi, wakulima na wadau wengine kutembelea Banda la MBIFACU lililopo katika Kijiji cha ushirika kwenye viwanja vya Nanenane Dodoma.
