JAMII YASISITIZWA KUIMARISHA FAMILIA KAMA MSINGI WA KUDUMISHA AMANI KWENYE JAMII



Wito umetolewa kwa Jamii kutunza na kuimarisha Familia kwani ndiyo msingi mkuu wa amani, upendo, na utulivu katika jamii na taifa kwa ujumla, ikitajwa kama nguzo ya upendo, heshima na darasa la maadili mema katika kuzalisha raia wema wanaopenda na kulinda amani kwenye jamii.

Wito huo umetolewa leo Jumatatu Aprili 06, 2026 na Diwani wa Viti Maalum Halmashauri ya Jiji la Dar Es salaam Mhe. Yusta Kinyukusu Kasamia na Bw. Ally Karim Mbiku, Mkazi wa Karume Jijini Dar Es Salaam, wakisema familia imara ni darasa la kufundisha watoto thamani ya maadili, amani, na upendo, ambayo ni msingi wa Taifa na jamii yenye maelewano.

"Tuna wajibu wa kulea na kutunza watoto, kuwalea katika malezi sahihi, tuwafuatilie na kuwa nao karibu ili waweze kuwa vizuri kimaadili. Mtoto akiwa na maadili tangu nyumbani hata kwenye jamii atakuwa na maadili mazuri na kubwa zaidi ni kumshirikisha Mungu katika hili kwani Vijana wengi waliokata tamaa ya maisha ndio hawa wanaokuwa chachu ya kufanya uhalifu lakini Kijana aliyefundishwa hatafikiria kuhusu uhalifu au kukaidi amri yoyoye na ndio watakaolinda amani yetu pia." Amesema Mhe. Kasamia.

Kwa upande wake Bw. Mbiku amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kaa kuunda tume ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani wakati na baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025, akisisitiza umuhimu wa Vijana kujiepusha na kufuata mikumbo na kujihusisha na matukio ya uvunjifu wa amani, akitaka kila mmoja kutambua thamani ya amani katika ustawi na maendeleo yao binafsi na ya Taifa.

Post a Comment