Na. Fullshangwe Blog, Mwanza
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, amesema kuwa Serikali inalenga kuona meli ya MV NEW Mwanza haitumiki tu kwa usafiri wa abiria na mizigo bali pia kama fursa muhimu ya kukuza utalii na biashara katika Ukanda wa Ziwa.
Amesema kuwa watalii wanapaswa kutumia meli hiyo kufika katika maeneo mbalimbali ya utalii kama Serengeti, Rubondo na Burigi Chato, huku akisisitiza kuwa Mwanza ni eneo la kimkakati kutokana na miundombinu ya usafiri wa anga inayoendelea kuboreshwa.
Aidha, amebainisha kuwa meli hiyo inaweza kutumika kwa shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo malazi, sherehe na hafla mbalimbali, jambo linaloweza kusaidia kupunguza msongo wa mawazo kwa wasafiri.
Pia ameongeza kuwa uwepo wa meli hiyo unafungua fursa za biashara katika sekta za madini, mazao na mifugo pamoja na kurahisisha usafirishaji kati ya Tanzania na nchi jirani kama Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na Sudan Kusini.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Ndg, Gerson Msigwa, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkoa wa Mwanza, leo Machi 22, 2026, katika Bandari ya Mwanza South, jijini Mwanza